I made this widget at MyFlashFetish.com.

DarLeo

Usikubali kupitwa na Darleo kila siku jioni kwa Habari na matukio ya leo leo. Gazeti pekee la kila siku jioni. Sasa limesheheni habari moto moto kutoka mtaani kwako.

Friday, September 17, 2010

Mzungu ndani ya daladala

Na Selma Steenhuisen na Athman Hamza.


"Nikiwa mmoja kati ya wakazi wengi wa Jiji la Dar es Salaam tusio na usafiri wa binafsi, nimelazimika kutegemea daladala.
Muda wa msongamano barabarani siku zote hunipa hisia maalum. Kadri unavyokuwa na haraka ya kuwahi sehemu, ndivyo daladala linavyoenda taratibu na kadri unavyoomba upate siti upumzishe miguu iliyochoka, ndivyo unavyojiongezea uwezekano wa kupinda mgongo mpaka mwisho wa safari yako.
Ni vigumu kwa siku kupita ndani ya daladala bila kupata kitu cha kukumbuka," anasema  Selma Steenhuisen ambaye ni raia wa Uholanzi.

Dada huyu wa Kiholanzi ambaye amekuwa akija Tanzania kila msimu wa kiangazi tangu mwaka 2000, ndivyo alivyoanza  kutoa uzoefu wake wa usafiri wa daladala wakati akizungumza na gazeti hili.

Katika safu hii tutakuwa tunawaletea wasomaji wetu uzoefu wa wazungu na usafiri wa daladala, kitu ambacho kimekuwa kikiwafanya kupenda na kutosahau mikikimikiki ya usafiri huo katika maisha yao yote.


Safari ya Mtoni Mtongani-Kawe

Mwanadada huyo ambaye amekwenda hewani kisawa sawa, ananza simulizi zake kwa kusema "wakati napanda daladala konda alikuwa tayari katikati ya maonyesho ya kuchekesha kwani gari zima walikuwa wakiangua vicheko kutokana na uhodari wa konda huyo katika kufanya vibweka.

Kama mchekeshaji haswa akiwa jukwaani, abiria tukiwa kama watazamaji, abiria wakaanza kumtania kwamba hana ubavu wa kuongea na mzungu (yaani mimi) na hapo ndipo ukawa mwisho wa jeuri yake, mie nikakaa kimya nikisubiri kibweka cha mchekeshaji huyo hodari.

Haikuchukua muda ili aanze kukusanya nauli kutoka kwetu, alianza kibweka kingine kwa kusema,  "najua jinsi ya kuongea na mzungu, mimi siwaogopi hawa wazungu ni kama wanyama tu, hivyo siwezi kuwaogopa.

Unajua wanapotaka kusema 'nani' wanasemaje?, "whooff" (kama mbwa). whooof, whoof (yani kama mbwa tu)".

Kutokana na vibweka hivyo vya konda, abiria wa basi zima waliangua kicheko na kufanya nami pia nishindwe kujizuia. Wakati naangua kicheko, abiria nao wakazidi kucheka baada ya kugundua nami nimeelewa.

Usipitwe na makala haya. Wiki ijayo tutakuletea safari ya njia nyingine. Kumbuka ni kila Alhamisi.

Njemba yataka kufanya mapenzi ndani ya daladala *lililewa chakari*

Na Godfrey Ismaely, jijini

MKAZI mmoja wa jijini ambaye alikuwa amepanda daladala lenye namba za usajili T169 ASY aina ya DCM ambalo lilikuwa linafanya safari zake kati ya Mbagala na Buguruni, jana alisababisha tafrani katika daladala hilo baada ya kuanza kuwapiga busu abiria wasichana.

Tafrani hiyo ilijitokeza saa 11:30 jioni ambapo daladala hilo lilikuwa likiendelea na safari zake za kawaida ndipo njemba huyo ambaye alikuwa amelewa chakari,  alianza kuangaza macho kwa kila abiria, akiwa amesimama.

Ghafla katika viti vya nyuma aliwaona kinadada watatu ambao walikuwa ni ndugu, bila kujali kuwa kitendo hicho ni aibu, aliwasogelea na kuanza kusema sema hovyo.

"Toto's mbona kimya au mfungo wa Ramadhan umewanyima raha? kama ndio hivyo mimi subiri niwape raha" bila kujali alianza kuwapiga busu mmoja baada ya mwingine," ililalamika njemba hiyo.

Aliendelea kulalamika, "mimi kama ni fedha nimewekeza kweli katika mfungo wote wa Ramadhan, so what i need it's only toto's who will spend all money which had save for holy Ramadhan month so still smile, ok. Kama nimelewa nimelewa kwa sababu leo ninazo fedha, unaziona hizi noti za sh. 10,000, zipo saba mimi si tajiri".

Aidha baada ya wafanyakazi wa daladala hilo kushuhudia hali hiyo, waliwataka kinadada hao kutulia bila kubishana na njemba hiyo, lakini bila ya kujali aliendela na vituko vyake hivyo.

"Abiria wangu, ninawaombeni mtulie, hivi ni baadhi tu ya vituko vinavyotokea katika kazi zetu hizi za daladala hivyo huyo jamaa msibishane naye na atashuka muda si mrefu kwani bado kidogo tufike mwisho wa kituo," alitahadharisha kondakta wa daladala hilo aliyejitambulisha kwa jina la Ramadhan Mohamed.

Hata hivyo, baada ya njemba huyo kuona kuwa abiria wote wameanza kumjadili ili kutafuta namna ya kumdhibiti kutokana na kuwadhalilisha wasichana hao,  alipofika katika kituo cha TAZARA, alishuka huku akiwa anapiga kelele, "mkojo....unanibana au nikojoe humu ndani....".